Monday , 6th Oct , 2014

Wizara ya Mawasiliano, sayansi na Teknolojia nchini Tanzania imesema matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano katika mikutano mbalimbali ya serikali, itasaidia kuokoa mamilioni ya fedha ambayo yangetumika katika sekta nyingine za maendeleo.

Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia nchini Tanzania Profesa Makame Mnyaa Mbarawa.

Waziri wa wizara hiyo Prof. Makame Mnyaa Mbarawa, amesema hayo wakati akizindua utaratibu mpya wa kufanya mikutano kwa kutumia video kwa taasisi za serikali nchini, ambapo amesema kufikia mwezi Oktoba mwakani ofisi na Hospitali za wilaya zitakuwa zimeunganishwa katika mkongo wa taifa ambapo kwa upande wa Zanzibar mpango huo umekamilika na unasubiri kuanza.

Kwa upande wake, Mkuu wa mkoa wa Pwani Mwantumu Mahiza aliyeshiriki katika mkutano kwa njia ya Video kutoka mkoani Pwani amesema serikali iboreshe na kuweka mkazo zaidi katika shule na vyuo mbalimbali ili kupunguza usumbufu na gharama za walimu pindi wanapokuwa pungufu

Katika hatua nyingine, serikali ya Tanzania imesema kujengwa kwa bei nafuu kulingana na eneo zinakojengwa nyumba hizo kutasaidia kupunguza ujenzi holela hasa sehemu za vijini.

Akiongea jijini Dar es salaam Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi nchini Prof Anna Tibaijuka katika kuadhimisha siku ya makazi duniani yenye kauli mbiu 'Sauti Kutoka Makazi Duni' waziri Tibaijuka amezitaka halmashauri zote nchini zipime viwanja kwa ajili ya kujenga nyumba za bei nafuu, ili kusaidia wafanyakazi wageni wanaopangwa kufanya kazi katika maeneo hayo.