Wednesday , 17th Feb , 2016

Tanzania imesema haina mpango wa kujitoa katika mahakama ya kimataifa ya ICC na kutaka kufanyiwa marekebisho ya baadhi ya vipengele vinavyolalamikiwa kuwa haitendi haki na imekuwa ikiwaonea viongozi wa bara Afrika.

Waziri wa mambo ya nje, ushirikiano wa Afrika Mashariki wa kikanda na kimataifa balozi Agustine Mahiga

Akizungumza na waandishi wa habari kuhusu siku mia moja za raisi Magufuli na serikali ya awamu ya tano, waziri wa mambo ya nje, ushirikiano wa Afrika Mashariki wa kikanda na kimataifa balozi Agustine Mahiga amesema ushindi wa rais wa Kenya,Uhuru Kenyata na makamu wake William Ruto umedhihirisha kuwa waafrika wanaweza kuishinda mahakama hiyo, na kusisitiza kuwa baadhi ya vipengele vilivyowekwa lazima vitazamwe upya.

Aidha akizungumzia siku 100 za serikali ya awamu ya tano, Balozi Mahiga amesema mafanikio mengi yamepatikana katika kuimarisha siasa za kimataifa ikiwemo kuleta maridhiano katika kulijadili mgogro wa Burundi, kuitangaza Tanzania kimataifa pamoja na kuweka wazi misiamo ya Tanzania iliyosaidia kuwa na nguvu ya pamoja na nchi marafiki katika kutatua changamoto zilizopo nchni.

Aidha Balozi Mahiga amesema rais Dkt. John Pombe Magufuli anatarajiwa kuhudhuria mkutano wa kimatifa wa marais wa nchi za Afrika Mashairiki unaotarajiwa kufanyika mapema mwishoni mwa mwezi huu mjini Arusha, ambapo Tanzania ni mwenyekiti wa mkutano huo unaolenga kujadili swala la kudumisha ushirikiano ndani ya nchi wanachama na changamoto zinazojitokeza.