Tuesday , 16th Dec , 2014

Wakati Watanzania wakiwa bado wanasubiri uamuzi ya serikali juu ya mapendekezo ya Bunge kuhusu sakata la akaunti ya Tegeta Escrow, wananchi wa ngazi mbalimbali wameendelea kuzungumzia suala hilo.

Wananchi hao wameiomba serikali kuhakikisha kuwa taratibu za sheria zinachukua nafasa yake bila kumuonea mtu wala kuingiliwa na siasa na wanaothibitika pamoja na kuwajibishwa wachukuliwe hatua zaidi zikiwemo adhabu za mfano.

Miongoni mwa waliotoa mapendekezo yao juu ya sakata hilo ni pamoja na Waziri Mkuu mstaafu, Mheshimiwa Fredrick Sumaye, ambaye amedai kuwa tatizo lililopo kwenye Wizara ya Nishati na Madini lipo pia katika wizara nyingine .

Wengine waliozungumzia sakata hilo ni pamoja na baadhi ya wasomi akiwemo Dakta Honest Ngowi na Bwana Doita Nanyaro, ambao wanaishauri serikali na vyombo vingine, kutumia sakata hilo kupanua mtandao wa kushughulikia matatizo kama hayo katika maeneo mengine yaliyokithiri kwa ubadhilifu na kuelekeza nguvu kushughulikia vyanzo vyake badala ya kusubiri matokeo ya matatizo .