Wednesday , 4th Nov , 2015

Viongozi wa madhehebu mbalimbali ya dini katika mkoa wa Kagera wameiomba serikali kuchukua hatua za haraka ili iweze kudhibiti vitendo vya mauaji ya kikatili yaliyotawala mkoani humo.

Padre Faustine Kamugisha Paroko wa kanisa kuu jimbo la Bukoba

Viongozi hao wametoa kauli hiyo wakati wakilaani vitendo vya mauaji ya kikatili vinavyoendelea kutokea mkoani Kagera, na kusema kuwa vitendo hivyo vinahatarisha amani na usalama wa maisha ya wananchi na vinapoteza nguvu kazi.

Aidha viongozi hao wamewaomba wale wanaojihusisha na vitendo hivyo waachane navyo badala yake wamrudie mungu na kurejesha hali ya amani na Usalama katika eneo hilo.

Nao baadhi ya wadau mbalimbali wa maendeleo katika mkoa huo wanaelezea athari za mauaji hayo kwa kusema kuwa yanachangia kudumaza kasi ya maendeleo ya jamii na kiuchumi kwa kuwa wakati mwingine yanawapelekea wananchi kutojihusisha na shughuli za uzalishaji mali kwa kuhofia usalama wa maisha yao na pia yanachangia kuwakatisha tamaa wawekezaji wenye nia kuwekeza mkoani humo.

Vitendo vya kuwaua watu kwa kuwakata kwa mapanga vilianza kutokea mwaka jana mwezi Juni hadi sasa zaidi ya watu ishirini wamekwishauawa kwa kukatwa katwa na mapanga, wanaouawa mara kwa mara wanakuwa wamekatwa sehemu ya shingo.