Thursday , 9th Oct , 2014

Mkuu wa Wilaya ya Ilala, mkoani Dar es salaam Bw. Raymond Mushi amewatahadharisha watanzania wanaougua magonjwa ya macho, dhidi ya hatari ya kuwa vipofu.

Tahadhari hiyo imetolewa wakati ambapo takwimu zinaonesha kuwa wakazi zaidi ya laki 4 katika jiji la Dar es salaam pekee wanaougua magonjwa ya macho ambayo yamepelekea kutoona vizuri na hatimaye kuwa vipofu.

Mkuu wa wilaya ya Ilala ametoa kauli hiyo leo jijini Dar es salaam wakati wa maadhimisho ya siku ya afya ya macho duniani yaliyoadhimishwa katika viwanja vya mnazi mmoja ambapo wakazi mbalimbali wa jiji walijitokeza kwa ajili ya kupima macho na kupatiwa ushauri wa namna ya kupata matibabu iwapo atagundulika kuwa na matatizo ya macho.

Aidha Mushi amesema kuwa kuna mahusiano makubwa kati ya ugonjwa wa kisukari na afya ya macho na kushauri watanzania kuwa na tabia ya kupima afya zao mara kwa mara ili kuona iwapo wanaugua ugonjwa wa kisukari ambao umekuwa ukichangia mtu kuwa na uono hafifu.

Aidha katika hatua nyingine, serikali imesema ina mpango wa kuongeza mahabusu za watoto katika maeneo mbalimbali nchini ili kuondokana na kukithiri kwa vitendo vinavyohusiana na unyanyasaji wa watoto ili kuwajenga watoto hao katika maadili bora.

Hayo yamesemwa leo jijini Dar es salaam na Kamishna wa Ustawi wa Jamii Danford Makala ambapo amesema kwa sasa zipo mahabusu Sita tu za watoto ambapo ameeleza mkakati uliopo ni kuziongeza katika maeneo mengi nchini ili kuwasaidia watoto.

kwa upande wake afisa mfawidhi msaidizi wa mahabusu ya Upanga Bi Zuhura Mfinanga amesema zipo changamoto nyingi wanazokumbana nazo katika kushughulikia watoto waliopo kwenye mgogoro wa sheria ikiwemo suala la usafiri kwa watoto hao kutoka kituoni hapo kwenda mahakaman na kuomba serikali iweke jitihada za kuongeza mahakama za watoto, mahabusu za watoto na shule za maadilisho ya watoto watukutu.

Mfinanga ameongeza kuwa Kwa sasa nchi nzima ina mahabusu Sita za watoto, mahakama moja na shule ya maadilisho ni moja tu.