Friday , 27th Jun , 2014

Serikali ya Tanzania imesema kuwa haiko tayari kuona baadhi ya watu wanaipotosha jamii ya viziwi Tanzania kwa kujifanya ni wakalimani wa lugha ya alama.

Waziri wa afya na ustawi wa jamii nchini Tanzania Dkt Seif Rashid.

Kauli hiyo imetolewa na waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk, Seif Rashid wakati akizungumza kwenye mkutano Mkuu wa Chama cha Viziwi Tanzania (Chavita) mkutano uliofanyika mjini Dodoma.

Dk, Rashid amesema kuwa wakalimani wa lugha za alama kwa viziwi ni kiungo muhimu sana katika mawasiliano hivyo mtu kutoa ukalimani wa lugha ya alama kwa kupotosha atachukuliwa hatua kali za kisheria.

Aidha, serikali imesisitiza kuwa imeondoa michango ya shule iliyokuwa ikichangiwa hapo awali isipokuwa kamati pamoja na bodi za shule zimepewa fursa ya kupanga michango ya shule zao inayohusu maendeleo kupitia vikao vyao.

Naibu waziri wa nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), anayeshughulikia Elimu, Mhe. Kassim Majaliwa, amesema hayo mjini Dodoma wakati akijibu swali la nyongeza la mbunge wa ubungo, Mhe.John Mnyika aliyetaka kufahamu kauli ya serikali kuhusu michango inayoendelea kutozwa mashuleni.

Mhe Majaliwa amesema wameziagiza kamati pamoja na bodi za shule hizo kuzingatia hali ya kipato cha walezi na wazazi wa wanafunzi katika kupanga michango hiyo kupitia vikao vyao ili kuepukana na michango hiyo kuwa kero kwa wananchi.