Monday , 8th Feb , 2016

Serikali imeyataka makampuni yanayoagiza na kuingiza nchini mafuta ya petroli, kulipa deni ambalo kampuni hizo zinadaiwa na serikali vinginevyo serikali itasitisha huduma za makampuni hayo mara moja.

Waziri wa viwanda, biashara na uwekezaji Charles Mwijage

Waziri wa viwanda, biashara na uwekezaji Charles Mwijage, ametoa agizo hilo jijini Dar es Salaam leo na kutaja kiasi halisi ambacho serikali inayadai makampuni hayo kuwa ni fedha za Tanzania takribani shilingi bilioni nne.

Waziri Mwijage amesema deni hilo linatokana na huduma iliyotolewa na serikali kwa makampuni hayo, mojawapo ikiwa ni huduma ya upimaji na upitishaji mafuta katika miundombinu ya kituo cha kushushia mafuta cha KOJ kilichopo Kurasini jijini Dar es Salaam.

Pasipo kutoa muda wala kutaja makampuni yanayodaiwa; Waziri Mwijage amesema kitendo cha kukaa na pesa za serikali kwa muda mrefu hakikubaliki, kwani kwa namna moja ama nyingine kampuni hizo zimekuwa zikikwamisha uwezo wa serikali wa kutoa huduma bora kwa wananchi wake.