Thursday , 4th Apr , 2019

Askari polisi wa kituo cha Polisi wilaya ya Kahama H1363, PC Gideon Clement (30) mkazi wa Muleba mkoani Kagera, amejiua kwa kujipiga risasi shingoni leo Alhamis Aprili 4, 2019 majira ya saa moja nusu asubuhi wakati akiwa kwenye lindo mjini Kahama.

Gideon Clement enzi za uhai wake.

Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga, ACP Richard Abwao amethibitisha kutokea kwa tukio hilo ambapo amesema sababu za askari huyo kujiua ni kutokana na kutofanikiwa kupata mtoto licha ya kuishi kwenye ndoa  na mkewe kwa muda wa miaka mitano.

"Sababu za kujiua kwake ameeleza kwa ujumbe aliotuma kwa mke wake kwamba hana sababu za kuendelea kuishi kwa sababu hajajaliwa kupata mtoto na amekaa kwenye ndoa kwa muda wa miaka mitano na mke wake ambaye ni mwalimu na inasemekana jana alilalamikia sana jambo hilo na alianza kuonesha dalili kwa kumtumia mkewe ujumbe wa simu akieleza kuhusu mali zake vikiwemo viwanja viko wapi", ameeleza Kamanda Abwao.

Kamanda Abwao amesema taratibu za kusafirisha mwili wa marehemu kwenda Muleba kwa ajili ya mazishi zinaendelea.