Sunday , 13th Jul , 2014

Rais Jakaya Kikwete wa Tanzania amesema muundo wa serikali utakaoamuliwa katika katiba ijayo ndio utakaoamua iwapo uchaguzi mkuu wa Rais na wabunge utafanyika mwakani au hautofanyika.

Rais wa Tanzania Dkt Jakaya Mrisho Kikwete.

Rais Kikwete amesema hayo katika kikao cha majumuisho ya ziara yake ya kuutembelea mkoa wa Tanga, ambapo amesema hatma ya chaguzi hizo inategemea matokeo ya mchakato wa katiba.

Akifafanua kuhusu kauli hiyo, Rais Kikwete amesema uchaguzi huo utaweza kufanyika mwakani iwapo rasimu itapitisha kuendelea kwa muundo wa serikali mbili yaani ya Muungano na ile ya Zanzibar.

Rais Kikwete amesema mojawapo ya mambo yatakayokwamisha uchaguzi mkuu ujao ni suala la serikali tatu kwani matokeo hayo yatahitaji muda mrefu wa kufanya maandalizi ya uchaguzi utakaoendana na matakwa ya serikali tatu.

Akifafanua zaidi, Rais Kikwete amesema hoja ya serikali tatu ikipita ni lazima kufanyike mchakato wa katiba yake, jambo ambalo amedai haliwezekani kulingana na muda uliopo kikatiba wa kufanya chaguzi za serikali za mitaa, na uchaguzi mkuu wa Oktoba mwakani.