Rais Magufuli na mkewe mama Janeth Magufuli wakisali katika moja ya makanisa aliyotembelea leo.
Rais Magufuli ametoa ujumbe huo mara baada ya kusali ibada ya Jumapili katika Kanisa Katoliki la Bikira Maria Parokia ya Chato, na baadaye kutembelea Kanisa la Anglikana la Mtakatifu Stephano Parokia ya Chato, Kanisa la African Inland Church la Chato na kumalizia katika Msikiti wa Omar Bin -L-Khattab wa Chato.
Dkt. Magufuli amesema pamoja na Watanzania wote kuungana kuombea amani na utulivu pia hawana budi kutekeleza kwa vitendo Maandiko Matakatifu ya Biblia yasemayo "Asiyefanya kazi na asile" kwa kuhakikisha kila mmoja anachapakazi kwa juhudi na maarifa ili kuharakisha maendeleo ya Taifa.
"Ndugu zangu nawashukuru sana, muendelee kuliombea taifa hili, taifa letu ni la umoja, sisi wote ni Watanzania, tuendelee kumuomba mola wetu, kudumisha amani yetu, kujenga umoja wetu kwa dini zote, makabila yote na vyama vyote, kwa sababu mola wetu anatupenda sisi sote" Amesema Rais Magufuli.
Aidha, mara baada ya kuwasalimu waumini wa Kanisa Katoliki la Bikira Maria Parokia ya Chato, Rais Magufuli ameendesha harambee ya kuchangia ujenzi wa jengo jipya la Kanisa hilo ambapo amefanikiwa kukusanya Shilingi Milioni moja za papo kwa papo.
Tayari Dkt. Magufuli alishachangia ujenzi huo kwa kutoa Shilingi Milioni kumi tarehe 03 Aprili, 2016 na ametoa wito kwa watu mbalimbali kujitokeza kuchangia ujenzi wa Kanisa hilo.
Katika Msikiti wa Omar Bin-L-Khattab na Makanisa ya Anglikana na African Inland Church Rais Magufuli amechangia Shilingi Milioni tano kwa kila moja kwa ajili kuendeleza na kukarabati majengo.



