Wednesday , 23rd Mar , 2016

Bodi ya Korosho Tanzania (CBT) imekiri kuwapo kwa changamoto ya upatikanaji wa pembejeo za kutosha za zao hilo kwa wakulima, huku wengi wao wakiamini kuwa upo uwezekano wa kupata pembejeo za ruzuku kwa asilimia 100.

Zao lac Korosho

Akizungumza Mkoani Mtwara katika kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC), Mkurugenzi wa Bodi hiyo, Mfaume Juma, amesema bajeti ya pembejeo za ruzuku inapitishwa na wadau wa zao hilo katika mkutano wa wadau ambao unafanyika kabla ya kuanza kwa msimu mpya.

Mfaume amesema kuwa Changamoto waliyokuwa nayo ni wakulima kutegemea zaidi pembejeo za kupewa na kukopeshwa na pindi zinapochelewa basi uzalishaji unapungua kwa kiasi kikubwa.

Aidha, amesema bodi itasimamia uuzwaji wa pembejeo hizo na kuhakikisha haziuzwi kwa bei ya soko ili mkulima aweze kunufaika na ruzuku ambapo kutakuwa na mpango rasmi wa kuhakikisha hilo linafanyika kikamilifu na kuwashinda walanguzi.