Tuesday , 29th Sep , 2015

Mkuu wa mkoa wa Arusha, Daud Ntibenda amewaagiza wasimamizi wa uchaguzi katika mikoa ya Arusha na Manyara, kuhakiki vifaa vya kupigia kura kama vipo sahihi kulingana na idadi ya wapiga kura, ili kuepusha kuahirishwa kwa uchaguzi kwa baadhi ya vituo.

Mkuu wa mkoa wa Arusha, Daud Felix Ntibenda

Agizo hilo ametoa jana jijini Arusha, wakati akifungua mafunzo ya siku mbili ya wasimamizi wa uchaguzi wa mikoa ya Manyara na Arusha, ambao wamekutanishwa kwa lengo la kubadilishana uzoefu na kusisitizwa umuhimu wa kusoma na kuzifahamu sheria za uchaguzi na kanuni zake, ili wasimamie kwa haki uchaguzi mkuu wa Rais, Ubunge na Udiwani.

Amesema kuwa uchaguzi uliopita wa mwaka 2010, kulikuwa na changamoto ya kuahirishwa kwa uchaguzi kwa baadhi ya vituo, sababu ya wasimamizi kutokagua vifaa vya kupigia kura mapema, mara wanapopokea toka tume ya taifa yauchaguzi na wanapofanya hivyo siku ya kupiga kura na kukuta upungufu huo, unaleta dosari.

Pia amehimiza umuhimu wa tume ya taifa ya uchaguzi kusambaza vipeperushi vya kuelimisha wapiga kura umuhimu wa kupiga kura na kutoa magari ya matangazo kutangazia wananchi umuhimu huo ili apatikane kiongozi bora na sio bora kiongozi.

Naye Katibu tawala wa Mkoa wa Arusha (RAS), Adoh Mapunda amesema Arusha kampeni zinaendelea vizuri, japo kuna upinzani mkali, ila kampeni ni za kistaarabu na hakuna vurugu kama baadhi ya watu wanavyosema.