Tuesday , 3rd Jun , 2014

Zaidi ya wanafunzi 3,402 wa Taasisi Teknolojia Dar es Salaam (DIT) wameendelea kugoma kufanya mitihani ya muhula wa mwisho wa mwaka wakishinikiza uongozi wa taasisi hiyo kuwaruhusu wenzao waliozuliliwa kufanya mitihani hiyo.

Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi nchini Tanzania Dkt Shukuru Jumanne Kawambwa.

Mgomo huo ambao umedumu kwa siku mbili sasa, umetokana na Uongozi wa taasisi hiyo kuwazuia zaidi ya wanafunzi 180 kufanya mitihani hiyo kutokana na kutokamilisha taratibu za ulipaji ada.

Akizungumza na East Africa Radio Afisa Uhusiano wa Taasisi hiyo Amani Kakana amesema ni utaratibu wa taasisi hiyo kuwa wanafunzi wasiolipa ada kutotambulika na chuo kutokana na kukosa usajili hivyo kutoruhusiwa kufanya mitihani.

Kwa upande wake rais wa serikali ya wanafunzi wa DIT Himida Elihuruma amesema wapo wanafunzi ambao wamelipa ada na kufanya usajili lakini hawajapewa namba kwa ajili ya mitihani hiyo, hivyo kuwaathiri wanafunzi, ambapo nao baadhi ya wanafunzi wa chuo hicho wamesema hawatofanya mitihani hiyo mpaka wenzao watakaporuhusiwa kufanya mitihani.