Wednesday , 25th Mar , 2015

WATU wawili wamefariki dunia, akiwemo mfanyabiashara mmoja maarufuc jijini Arusha, aliyefia kwenya Klabu ya wafanyakazi wa benki Kuu ,BOT, tawi la Arusha, na mwingine ambae hajafahamika, aliokotwa akiwa amesokomezwa mtaroni.

Kamanda wa jeshi la Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas

Kamanda wa jeshi la Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas, amemtaja mfanya biashara huyo kuwa ni Obed Masawe, (50) ambae anamiliki duka la kuuza vinywaji vikali ,maarufu Masobe Treders, lililopo jengo la Chama cha Mapinduzi CCM, Mkoa wa Arusha.

Amesema mfanyabiashara huyo ambae ni mkazi wa Njiro jijini Arusha,alifikwa na mauti akiwa kwenye klabu ya wafanyakazi wa Benki kuu ya Tanzania, BOT,alipokuwa akiendelea kunywa bia.

Sabasi amesema tukio hilo limetokea Machi 23 mwaka huu, majira ya saa 1.30 usiku,ghafla alijisikia vibaya, na taarifa za awali zinaonyesha kuwa alikuwa akisumbuliwa na ugonjwa wa presha.

Katika tukio lingine Kamanda, Sabas, amesema mwanamke mmoja anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 18 hadi 25, alikutwa amefariki dunia na mwili wake kusokomezwa kwenye mtaro wa maji ya mvua jana, katika makutano ya bara bara ya Makongoro na Azimio, jirani na jengo
la CCM Mkoa.

Amesema mwili wa marehemu huyo umehifadhiwa hospital ya mkoa ya Mount Meru, ukisubiri ndugu kujitokeza kumtambua.

Ameongeza kuwa marehemu huyo ambae hajafahamika, mwili wake uligundulika baada ya kutoa harufu .

Uchunguzi unaendelea kufahamu vyanzo vya vifo hivyo.