Wednesday , 24th Feb , 2016

Waziri wa nchi Ofisi ya Rais tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI),Mhe. George Simbachawene ameziagiza halmashauri zote nchini kuanza mara moja kulipa malimbikizo ya madeni ya watumishi hususani walimu.

Waziri wa nchi Ofisi ya Rais tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI),Mhe. George Simbachawene

Waziri simbachawene ametoa agizo hilo mkoani Morogoro wakati wa kikao cha kazi kilichoshirikisha wakuu wa wilaya, wakurugenzi na wakuu wa idara wa halmashauri zote za mkoa huo ambapo pamoja na mambo mengine amesema serikali haitawavumilia watendaji wanaoisababishia hasara na kusisitiza uadilifu na uwajibikaji katika kuwahudumia wananchi.

Waziri huyo wa Tamiesemi pia ametoa onyo kwa maafisa utumishi pamoja na wahasibu wa halmashauri hizo kuacha tabia ya kutengeneza madai feki ya watumishi na kuisababishia serikali hasara.

Aidha waziri Simbachawene amezitaka halmashauri hizo kuhakikisha zinasimamia vyema sera ya serikali ya kutoa huduma ya matibabu bure kwa wazee ili kuondoa malalamiko kwa wagonjwa huku akiiagiza halmashauri ya Morogoro kufikia mwezi juni mwaka huu kuhamishia ofisi zote katika eneo lililopangwa la mvuha.

Nao baadhi ya wakurugenzi wa halmashauri hizo wakiwasilisha taarifa za maendeleo za halmashauri zao wameeleza mikakati waliyonayo ya kuhakikisha halmashauri hizo zinakusanya mapato ya kutosha ili kuipunguzia mzigo serikali wa kuzihudumia halmashauri hizo.