Wednesday , 3rd Apr , 2019

Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Profesa Mussa Assad amesema hafikirii kufanya maamuzi yoyote kutokana na kitendo cha Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuadhimia kutofanya naye kazi.

CAG Profesa Mussa Assad

Profesa Assad amesema hayo leo Jumatano Aprili 03, 2019 wakati akizungumza na Television ya Taifa (TBC) kwa njia ya simu.

Akijibu swali la Mtangazaji aliyetaka kujua kama anaweza kuchukua maamuzi magumu kutokana na hatua iliyochukuliwa na Bunge, CAG Assad amesema kwamba hana maamuzi yoyote atakayoweza kuchukua.

Amesema kwamba yeye ana majukumu ya kikatiba yanayomsubiri kuyatekeleza kwamba ataendelea kutekeleza kama kawaida.

"Ninachokifanya mara nyingi hapa ni kuomba dua tu basi. Watu waongozwe vizuri wafanye maamuzi ambayo yana faida kwa nchi hii. Mimi sina acha kufanya. Nina majukumu yangu ya Kikatiba ya kufanya".

Pamoja na hayo Profesa Assad ametoa rai kuwa hansadi ya maswali na majibu kutoka katika mahojiano yake pamoja na Kamati ya Bunge ya Maadili iwekwe wazi ili kila Mtanzania ajue nini kilichozungumzwa baada ya kuitwa na kamati hiyo.