Ijumaa , 20th Sep , 2024

Hospitali ya Taifa ya Muhimbili imefanikiwa kuondoa uvimbe wa kilogram 5, zilizokuwa mwilini mwa Karume Ally Karume aliyekuwa mkazi wa Lindi ambaye alifika Dar es Salaam kwa ajili ya matibabu ya ugonjwa huo uliomtesa kwa miaka 26.

Karume Ali kabla ya upasuaji

Ugonjwa huo wa kurithi ulimuanza Karume kama vinundu kwenye mwili wake na baadaye ukaongezeka na kuenea maeneo mbalimbali mwilini wake na kumsababishia maumivu wazazi wake wanaelezea zaidi.
"Mwanangu hizi nyama zilimuanza akiwa na umri wa miaka 15 mpaka ambapo amepatiwa matibabu siku zote nimemlea mwenyewe bila baba nahangaika nae kila siku, hizo nyama zilikuwa zikianza kumuuma hadi anashindwa kulala tulikuwa tunakesha nae tunashukuru kwa matibabu haya aliyopatiwa", alisema Salma Karume, Mama wa mgonjwa.

"Tunashukuru sana waandishi wa habari kwa kulifanikisha hili kwa maana nyie nduio mmetufanikishia kupaza sauti kijana wetu akapata matibabu haya baada ya kuteseka kwa miaka mingi", alisema Salum Hidobelele, Mjomba wa mgonjwa.

"Asanteni sana kwa matibabu haya hali yangu ilikuwa mbaya sana japo sijapona kabisa lakini nashukuru kwa sababu tumeondoa sehemu kubwa ya uvimbe uliokuwa unanitesa", alisema Karume Karume, Mgonjwa.

Kwa upande wake mkuu wa kitengo cha upasuaji rekebishi katika idara ya upasuaji anaelezea ugonjwa huo na namna walivyompatia matibabu.
"Ugonjwa huu ni wakurithi na unawea kumpata mtu yeyote kwa maana unatokna na vina saba kizazi hadi kizazi, tulimpokea tarehe 24, Agost,2024 tukamtoa uvimbe kama ambavyo mmemkuta leo yupo vizuri japo atakuwa anakuja clinic za mara kwa mara kwa ajili ya kuangalia kidonda lakini ugonjwa huu ukiutambua mapema ni afadhali kabla tatizo halijawa kubwa kwahiyo wazazi wawe wanawaangalia watoto wao wanapozaliwa ili kupunguza ukubwa wa tatizo", alisema Dkt.Laurean Rwanyuma, Mkuu wa kitengo cha upasuaji rekebishi.

"Tumemfanyia upasuaji gharama ni shilingi milini 1.5 , ambayo anadaiwa hatukutaka kukatiza matibabu kwa ajili ya ukubwa wa tatizo tukaona tumtibie kwanza , kwahiyo nitoe wito kwa watanzania kusaidia kuchangia huduma za matibabu kwa control namba yetu kwa maana wahitaji wanaokuja ni wengi lakini hawaan uwezo wa kumudu gharama za matibabu", alisema Dkt.Rachel Mhavile, Mkurugenzi wa huduma za upasuaji.