Jumatano , 18th Sep , 2024

Viongozi wa Dini nchini wametakiwa kuwashauri waumini wao kurudi Hospitali kwa ajili ya vipimo kabla na baada ya kuwaombea kwani baadhi yao wamekuwa wakipoteza maisha kwa kuacha matibabu wakiamini wameponywa na maombi kumbe bado wana changamoto.

Dkt.Omary Ubuguyu, Mkurugenzi msaidizi magonjwa yasiyoambukiza, wizara ya Afya.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi msaidizi, magonjwa yasiyoambukiza Wizara ya Afya  Dkt. Omary Ubuguyu, akiongea na EATV, kuhusu umuhimu wa wanachi kujikinga na Magonjwa yasiyo ya kuambukiza.
“Tunachoshauri kwenye Ibada zao wawashauri wanapowaombea wakimaliza wawaambie warudi Hospitali kucheki kama tatizo bado lipo au limeisha sio kama wanamjaribu Mungu hapana bali ni kudhihirisha kama Afya zao zimerudi na kama bado basi waendelee na Dawa ili kuepusha hatari za kifo wanazoweza kuzipata wagonjwa baada ya kutoka kuombewa kwenye nyumba za ibada”, alisema Dkt.Omary Ubuguyu, Mkurugenzi msaidizi magonjwa yasiyoambukiza, wizara ya Afya.

Nao viongozi wa Dini wanaelezea majukumu yao ya kuwakumbusha waumini umuhimu wa matumizi ya Dawa.
“Ni kweli Mungu anaponya ndio maana ametoa maarifa ya kila ugonjwa iwepo Dawa yake ndio maana kuna madaktari ambao wamebobea kwenye magonjwa hayo na tutawashauri waumini kuzingatia maelekezo ya madaktari”, alisema  Mch. John Kamoyo, Mtumishi Kanisa la CCT.

“Mtume wetu alisema mtu huyo apelekwe kwa mganga kwa maana anajua kuna muda inahitajika zitumike Dawa kutokana na aina ya ugonjwa”, alisema Shekhe Hamis Mataka, M/kiti Halmashauri kuu BAKWATA.

Nao baadhi ya vijana waliopata magonjwa hayo wanaelezea namna walivyoyashinda magonjwa hayo.
“Niligundulika nina sickle cell, nikaanza majukumu matibabu na mpaka leo naendelea na maisha yangu pamoja na masomo yangu”, alisema Samwel  Maingu, Mgonjwa wa Sickle cell.

“Nilipojigundua nina Sukari nikaanza kutumia dawa na imenisaidia sasa hivi niko vizuri nawashauri wengine wakijigundua watumie dawa mapema kabla kabla hali haijawa mbaya”, alisema Gaudensia Nyeupe, Mgonjwa wa Kisukari.