Jumapili , 11th Aug , 2024

Maafisa wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa - NIDA kutoka wilaya zote mikoa ya Kagera na Kigoma wametakiwa kuhakikisha wanafanya utambuzi na kusambaza kwa wananchi husika vitambulisho vya Taifa 78,766 vilivyo tayari lakini vimekwama kwa muda mrefu kwenye ofisi za kata.

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani nchini, Daniel Sillo

Wito huo umetolewa na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani nchini, Daniel Sillo akiwa kwenye ziara ya katibu mkuu wa Chama Cha Mapinduzi - CCM, Dkt. Emmanuel Nchimbi kwenye mkutano wa hadhara Manispaa ya Bukoba mkoani Kagera.

Naibu Waziri Sillo amesema kuwa kupitia Wizara hiyo serikali ilitenga kiasi cha shilingi milioni 42.5 kwa ajili ya kuwezesha upatikanaji wa vitambulisho hivyo vya Taifa - NIDA ambapo kuanzia Oktoba 2023 vilianza kusambazwa nchi nzima.

"Naelekeza maafisa NIDA mikoa ya Kagera na Kigoma na wilaya zote katika mikoa hii kuhakikisha wanafanya uhakiki, utambuzi na usambazaji wa vitambulisho hivyo kwa wananchi wenye Sifa za kuvipata washuke hadi ngazi za chini wananchi wapate haki zao". Amesema Sillo.