Jumamosi , 11th Jul , 2020

Aliyekuwa Katibu Tawala (DAS) Wilaya ya Handeni Mkoani Tanga Boniface Maiga amepoteza maisha katika ajali huku watu watatu wakijeruhiwa akiwemo Mbunge wa jimbo la Handeni Omary Kigoda ambaye amevunjika vidole viwili vya mkono wa kulia wakati wakielekea kwenye mkutano mkuu jijini Dodoma.

Aliyekuwa Katibu Tawala (DAS) Wilaya ya Handeni Mkoani Tanga Boniface Maiga

Kwa mujibu wa taarifa yake Dereva wa gari la Mbunge wa Handeni Omary Kigoda, Peter Mganga amesema ajali hiyo imetokea majira ya saa saba usiku katika eneo la Vikonji Dodoma.

Dereva huyo amesema chanzo cha ajali hiyo imetokana na mwendo kasi aliokuwa nao dereva wa basi baada ya kuovateki sehemu yenye kona.

Dereva huyo wa Mbunge amesema baada ya dereva wa basi kuovateki katika eneo hilo lenye kona kali alimuwashia taa ili aweze kupunguza spidi ya gari ila dereva wa basi hilo hakupunguza spidi na ndipo wakavana uso kwa uso.

''Katika ajali hii dereva na kondakta wa basi wote wamefariki nilijaribu kumuwaahia taa nyingi ili apunguze spidi lakini cha kushangaza kama hajaziona ilibidi sisi tupaki pembeni ndipo mwendo aliokuwa nao ililazimu kulivaa gari letu hasa upande wa kulia aliokuwa amekaa mheshimiwa Mbunge na Das wetu aliyefariki,''amesema Mganga.

Amesema mara baada ya ajali hiyo Das alipoteza maisha hapo hapo huku wao wakikimbizwa katika hospitaliti ya Chamwino kwajili ya matibabu ambapo Mbunge alilazimika kufanyiwa upasuaji wa vidole hivyo wakahamishiwa katika hospitali ya Mkoa Dodoma (General Hospital).

Mganga amesema baada ya kupata matibabu wawili waliruhusiwa kutoka hospitalini hapo saa kumi na moja alfajiri huku Mbunge Kigoda akibaki kuendelea na matibabu ya vidole alivyoumia.

Amesema katika gari hiyo ya Mbunge Kigoda walikuwa watu wanne akiwemo yeye Dereva wa Mbunge Peter Mganga,  Mbunge Omary Kigoda, Mbelwa Saidy ambaye ni ndugu yao pamoja na Boniface Maiga (DAS) aliyepoteza maisha na kueleza kuwa mwili wa marehemu upo katika hospitali hiyo ya Mkoa.