Jumatatu , 27th Aug , 2018

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amedai amefarijika baada ya kuzungumza na msanii Ommy Dimpoz kwa njia ya simu kuwa anaendelea vizuri na kumuahidi kuungana naye katika mazoezi katika siku za hivi karibuni.

Ommy Dimpoz

Makonda amebainisha hayo kupitia ukurasa wa kijamii asubuhi ya leo, Agosti 27, 2018 baada ya kutolewa taarifa kwenye mitandao ya kijamii zikimuhusisha mwanamuziki huyo, kuzidiwa na kurudishwa tena hospitalini nchini Afrika Kusini kwa lengo la kupatiwa matibabu ya maradhi yanayomsibu.

"Jana saa 8 usiku nilipata muda wa kuongea na rafiki yangu Ommy. Nilifurahi sana kupiga stori na ndugu yangu hasa kujua anaendelea vyema na 'soon' tunarudi GYM", ameandika Paul Makonda.

Juni 15, 2018 msanii Ommy Dimpoz aliufahamisha umma kupitia 'video clip' yake fupi yenye takribani sekunde 55, kuwa amefanyiwa upasuaji mkubwa wa koo ambao ulimchukua takribani siku 15 hadi kupata nafuu huko nchini Afrika Kusini.

Kutokana na maradhi hayo yanayomsumbua msanii huyo, amekuwa kimya kwa kipindi kirefu kuonekana kwenye mitandao ya kijamii, hata watu kusikia sauti yake kwa namna yoyote ile ambayo wamezoea kuisikia kwa haraka.