Jumatano , 23rd Nov , 2016

Makamu wa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan, amesema, Serikali ya Tanzania imepiga hatua kubwa katika kulinda na kutetea haki za binadamu kwa kuzingatia maazimio mbalimbali ya ndani ya nchi na ya kimataifa ikiwemo haki ya kuishi.

Makamu wa Rais, akizindua Jarida la Mahakama ya Afrika

 

Mh. Samia ametoa kauli hiyo jijini Arusha kwa niaba ya Rais Dk John Pombe Magufuli wakati anafungua mkutano wa mazungumzo wa masuala ya demokrasia na haki za binadamu ya Mahakama ya Afrika ya Watu na Haki za binadamu.

Amesema Tanzania ni mfano wa kuigwa barani Afrika kwa kuzingatia na kutekeleza ipasavyo mikataba mbalimbali ya kimataifa inayolenga kuhakikisha wananchi wake wanapata huduma bora na za msingi ikiwemo huduma ya afya na elimu bila kubaguliwa kutokana na ulemavu,jinsia,rangi au dini.

Amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kutekeleza na kuzingatia matamko mbalimbali ya Dunia yanayolenga kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za kijamii ikiwemo haki ya kuishi.

Kwa upande wake, Rais wa Mahakama ya Afrika ya Watu na Haki za Binadamu Justice Sylvain Ore amesema kuwa mkutano huo ni muhimu kwani unalenga kujadili na kuweka mikakati inayolenga kuhakikisha nchi za Afrika zinazingatia na kulinda haki za bindamu hasa haki za wanawake kwa kiwango kikubwa.

Justice Sylvain Ore

Mkutano huo wa Mahakama ya Afrika ya Watu na Haki za Binadamu ambao unafanyika Jijini Arusha umehudhuriwa na wajumbe kutoka mataifa mbalimbali ya Afrika wakiwemo wajumbe kutoka Umoja wa Afrika AU na lengo la mkutano huo ni kutajadili masuala ya demokrasia na haki za binadamu katika nchi za Afrika.