Jumanne , 12th Jul , 2022

Klabu ya Simba inatarajiwa kuweka kambi ya wiki nne kwa ajili ya maandalizi ya msimu mpya wa mashindano wa 2022/23 katika mji wa Ismailia nchini Misri huku kikosi hicho kikitarajiwa kuondoka nchini mnamo Julai 14.

kikosi cha Simba

Meneja habari na mawasiliano wa klabu ya Simba Ahmed Ally amesema kambi hiyo itahusisha wachezaji wote waliosajiliwa na klabu hiyo kwa ajili ya msimu ujao wa mashindano huku baadhi ya nyota watakaoitwa Taifa Stars watachelewa kujiunga na kambi hiyo nchini Misri.

“Tutakuwa na wachezaji wote kasoro wale ambao watakuwa kwenye timu za Taifa ambao tutawaacha wakiwa na majukumu mengine na hivyo Agosti 15 tutarejea nchini kujiandaa na tamasha la Simba Day litakalofanyika Agosti 6 mwaka huu kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa , jijini Dar es Salaam ”amesema Ahmedy Ally

Katika hatua nyingine, Simba imemtambulisha kocha wake mkuu Zoran Maki aliyesaini kandarasi ya mwaka mmoja huku kukiwa na kipengele cha kuongeza mkataba endapo atafikia malengo yaliyowekwa kwenye mkataba wake.

“Zoran yupo hapa kuhakikisha Simba inapata ubingwa wa Ligi, Ngao ya Jamii na Kombe la Shirikisho pamoja na kuingia nusu fainali Caf,” amesema Ahmedy Ally