Jumamosi , 2nd Dec , 2017

Mabingwa watetezi wa ligi kuu soka Tanzania bara Yanga SC, imethibitisha kuwa itaanza mazoezi wiki ijayo kwaajili ya kujiwinda na mchezo wa raudni ya 12 dhidi ya Mbao FC.

Taarifa kutoka klabu ya Yanga imeeleza kikosi hicho kitarejea mazoezini kwenye uwanja wa Uhuru jijin Dar es salaam, Jumatatu ya Desemba 4 asubuhi baada ya mapumziko ya wiki moja kufuatia ligi kusimama kupisha michuano ya CECAFA Challenge.

Yanga tayari imeshafanya usajili wa nyota wawili kwenye kipindi hiki cha dirisha dogo lililofunguliwa tangu Novemba 15. Wachezaji hao ni mlinzi Fiston 'Festo' Kayembe Kanku kutoka DR Congo pamoja a Yohana Mkomola ambaye alifanya vizuri na Serengeti Boys.

Yanga inashika nafasi ya tatu ikiwa na alama 20 baada ya raundi 11, nyuma ya Simba SC na Azam FC zenye alama 22 kila mmoja zikitofautiana idadi ya mabao ya kufunga na kufungwa.