Jumatano , 26th Jun , 2019

Kuelekea michezo ya pili ya Kundi A kwenye michuano ya AFCON 2019 inayoendelea nchini Misri, timu ya taifa ya Uganda imekutana na viongozi mbalimbali kwenye kambi yake wakiwemo wa michezo na wa kimila.

Mfalme wa Tooro, Oyo Nyimba Kabamba Iguru Rukidi IV

Katika mazoezi ya timu hiyo ambayo leo itacheza mechi yake ya pili dhidi ya Zimbabwe baada ya kushinda mchezo wa kwanza dhidi ya DR Congo, ilitembelewa na mfalme wa moja ya falme tano zinazopatikana nchini Uganda.

Mfalme wa Tooro, Oyo Nyimba Kabamba Iguru Rukidi IV, alifika kwenye uwanja wa Arab Contractors jijini Cairo, ambapo alishuhudia mazoezi ya timu hiyo na kuwapa moyo wachezaji kuelekea mchezo wao wa leo.

Mbali na mfalme huyo Rais wa shirikisho la soka nchini humo (FUFA), Moses Hassim Magogo, naye jana amefika kambini na kuongea na wachezaji.

Moses Hassim Magogo ambaye alipigana na kuhakikisha Uganda inaanza maandalizi mapema ikiwemo kuweka kambi Abu Dhabi, aliwaeleza wachezaji wa The Cranes kuhakikisha wanajituma na kupata matokeo kama walivyofanya kwenye mchezo wa kwanza.