Jumanne , 13th Feb , 2018

Shirikisho la soka nchini TFF kupitia Kamati yake ya  Nidhamu imemfungia mechi tano na adhabu zingine mchezaji wa Kagera Sugar Juma Nyoso kwa kosa la kumpiga shabiki baada ya mechi.

Kamati hiyo ya TFF iliyokutana Jumamosi Februari 10, 2018 pia imempiga faini ya shilingi 1,000,000 (Milioni moja) mchezaji huyo, ambapo kikao hicho kimejiridhisha kuwa Nyoso alimpiga shabiki huyo.

Nyoso alimpiga shabiki baada ya mchezo wa ligi kuu soka Tanzania Bara kati ya timu yake ya Kagera Sugar dhidi ya Simba kwenye uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba mkoani Kagera.

Katika mchezo huo Kagera Sugar ilipoteza kwa mabao 2-0,  mabao ya Simba yakifungwa na Said Ndemla na John Bocco. Baada ya tukio hilo Nyoso alikamatwa na Polisi na kuwekwa ndani ambapo kesi yake bado inaendelea.

Nyoso amekuwa na matukio yasiyo ya kiungwana michezoni ambapo awali aliwahi kufungiwa miaka miwili kutojihusisha na soka baada ya kumshika makalio mshambuliaji John Bocco, kipindi akiwa Azam FC huku Nyoso akiwa Mbeya City.