Alhamisi , 25th Dec , 2014

Ligi ya kikapu ya mkoa wa Dar es salaam RBA mzunguko wa pili, inatarajiwa kuanza kuanza kutimua vumbi Januari sita mwakani uwanja wa ndani wa Taifa jijini Dar es salaam.

Akizungumza na East Africa Radio, Makamu wa Rais wa Chama cha mpira wa Kikapu Mkoa wa Dar es salaam BD, Richard Julles amesema Ligi ilisimama ili kupisha mashindano ya Taifa pamoja na mashindano ya vyuo ambayo yalishirikisha vilabu mbalimbali ambavyo ni shiriki vya Ligi ya RBA.

Julles amesema michuano hiyo inayotarajiwa kushirikisha vilabu takribani 12 itasaidia kuendelea kupata vijana watakaounda timu nzuri na ya muda mrefu ya taifa itakayoweza kushiriki mashindano mbalimbali ya ndani na nje ya nchi.

Julles amesema, baada ya kumalizika kwa RBA, chama kinajipanga kwa ajili ya maandalizi ya mashindano ya Taifa na Super Cup yanayotarajiwa kufanyika hapo mwakani yakiwa na lengo pia la kutafuta timu bora ya mwaka pamoja na kuibua vipaji vya vijana hapa nchini.