Jumamosi , 2nd Dec , 2017

Klabu ya Simba SC imethibitisha kuwa Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Dkt. Harrison Mwakyembe atakuwa mgeni rasmi kwenye mkutano mkuu wa klabu hiyo utakaofanyika kesho.

Mkutano huo mkuu maalum wa klabu utakuwa na Agenda moja tu ambayo ni kumtangaza mzabuni aliyeshinda kumliki sehemu ya klabu kupitia mfumo wa hisa ambao utaanza kutumika kuendesha klabu hiyo.

Taarifa iliyotolewa leo na klabu hiyo imeeleza kuwa, “Kwenye mkutano huu Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Dkt. Harrison Mwakyembe anatarajiwa kuwa mgeni rasmi”.

Simba tayari imeshapitia hatua mbalimbali za ubadilishaji wa uendeshaji na umiliki wa klabu ambapo serikali na shirikisho la soka nchini TFF vimebariki mabadiliko hayo kwa manufaa ya maendeleo ya soka nchini.

Mkutano huo maalum utafanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Mwalimu Nyerere jijini Dar es salaam na historia itaandikwa kwa mara ya kwanza katika soka la Tanzania.