Ijumaa , 11th Jul , 2014

Viwango vinavyoonyeshwa na wachezaji chipukizi wa klabu ya soka ya Yanga waliopandishwa kutoka kikosi cha vijana chini ya miaka 20 cha klabu hiyo wameonesha kumkuna kocha mkuu wa klabu hiyo Marcio Maximo

Kocha mkuu wa klabu ya Yanga Marcio Maximo akiwa na mshambuliaji Jerson Tegete.

Kocha mkuu wa klabu ya soka ya Dar es salaam Young Africans Mbrazil Marcio Maximo amesema ameridhishwa na viwango vya wachezaji chipukizi aliowapandisha katika kikosi cha kwanza cha timu hiyo ambacho kinaendelea na mazoezi katika uwanja wa shule ya sekondari ya Loyola jijini Dar es salaam

Maximo ameonesha imani kubwa kwa vijana hao 10 ambao hivi karibuni aliwapandisha katika kikosi cha kwanza ikiwa ni moja ya sera za kocha huyo ambaye kwakati akiifundisha taifa stars aliweza kuibua vipaji vya chipukizi wengi akiwemo mshambuliaji anayeng'ara na kalbu ya Yanga kwa sasa Jerson Tegete na Kigi Makasi ambaye kwa sasa yuko nje ya dimba baada ya kuwa majeruhi akiichezea klabu ya Simba

Aidha Maximo amesema ili timu yoyote iweze kufanikiwa ni lazima iwe na utaratibu wa kutumia vijana ambao watachanganyika na wakongwe suala ambalo linafaida kubwa kwa siku za usoni katika maendeleo ya soka kwa klabu husika na taifa kwa ujumla.