Jumanne , 25th Mei , 2021

Katika muendelezo wa michuano ya kombe la Shirikisho Azam Sports Federation Cup hatua ya Robo fainali, mchezo mmoja unachezwa leo wa hatua hiyo kati ya Mwadui FC dhidi ya Yanga SC katika dimba la CCM Kambarage huko Shinyanga, mchezo utachezwa Saa 10:00 Jioni.

Wachezaji wa Yanga wakiwa mazoezini kujiandaa na mchezo dhidi ya Mwadui

Yanga wanaingia kwenye mchezo huu wakiwa wanapewa nafasi kubwa zaidi ya kufuzu kuliko wenyeji wao Mwadui ambao hawajawa na msimu mzuri na tayari timu hiyo imeshashuka daraja kwa upande wa Ligi kuu soka Tanzania bara wakati Yanga wao wapo nafasi ya pili kwenye muondelezo wa VPL.

Kwenye mchezo wa mwisho timu hizi kukutana Yanga ilishinda mchezo kwa bao 5-0 mchezo ambao ulichezwa katika dimba la CCM Kambarage, ilikua Disemba 12, 2020. Na katika rekodi Mwadui hawajaifunga Yanga kwenye michezo mitano ya mwisho waliokutana wakitoka sare mchezo mmoja wakati Yanga wakishindi michezo minne kati ya hiyo.

Yanga walikata tiketi ya kucheza hatua hii baada ya kuitoa Tanzania Prisons kwa ushindi wa bao 1-0, mchezo ambao ulichezwa kataika Dimba la Nelson Mandela Sumbawanga, Rukwa, wakati Mwadui wao waliitoa Coastal Union kwa kuifungwa mabao 2-0.

Na mshindi wa jumla wa mchezo huu atafuzu kucheza hatua ya nusu fainali, na atacheza dhidi ya Biashara United ambayo ilishatinga hatua hiyo kwa kuitoa kwenye mashinda klabu ya Namungo ya Lindi kwa kuifunga mabao 2-0. Mchezo huo wa nusu fainali utachezwa uwanja wa Ali Hassan mkoani Tabora.