Jumatano , 13th Jun , 2018

Mchezaji wa timu ya Taifa ya Ubelgiji na klabu ya Chelsea, Eden Hazard ametabiri kuwa timu ya Taifa ya England itafika hatua ya fainali katika mashindano ya kombe la Dunia yanayofanyika nchini Urusi kuanzia kesho Juni 14, 2018.

Mchezaji huyo ametoa utabiri wake baada ya kupost katika mtandao wake wa kijamii wa Instagram na kuonesha, England itatinga fainali lakini itapoteza mchezo  huo kwa kufungwa na timu ya Ubelgiji katika mchezo wa fainali Julai 15, 2018.

Hazard ametabiri kwamba England itafanikiwa kumaliza nafasi ya pili kundi G kabla ya kuitoa Colombia hatua ya 16 bora, kisha kuifunga Ujerumani robo fainali na kuindosha Argentina hatua ya nusu fainali.

Mbelgiji huyo ameandika “Huu ni utabiri wangu wa kombe la Dunia 2018, marafiki zangu wengi  kutoka Chelsea, huu ni utabiri wangu, wako ni upi?”

England na Ubelgiji zimepangwa pamoja kundi G katika mashindano ya kombe la Dunia na zitakutana Juni 28, 2018 kuhitimisha michezo ya kundi hilo ambalo linajumisha timu za Panama na Tunisia.