Ijumaa , 16th Jul , 2021

Mshambuliaji hatari wa Klabu ya soka ya Simba, John Bocco ametwaa tuzo ya mchezaji bora wa Ligi Kuu Tanzania bara kwa mwezi Juni wakati Kocha wake Didier Gomes akitwaa tuzo ya Kocha bora wa mwezi huo.

Nahodha wa Klabu ya Simba, John Bocco ambaye ndiye mchezaji bora wa VPL kwa mwezi Juni akishangilia moja ya bao alilofunga katika mchezo wa Ligi kuu Tanzania Bara msimu huu.

Wawili hao walifanya vyema kwa mwezi huo walipoisaidia Simba kushinda mechi zote tatu dhidi ya Polisi Tanzania, Ruvu Shooting na Mbeya City zilizoifanya ikae kileleni mwa VPL  huku John Bocco akifunga mabao matatu katika michezo hiyo.

John Bocco ''Adebayor''ambaye ndiye kinara wa kupachika mabao katika Ligi Kuu,amewashinda wachezaji Feisal Salum ''Fei Toto'' wa Yanga  na Idd Seleman ''Nado'' wa Azam walioingia kwa pamoja katika kinyang'anyiro hicho wakati Didier Gomes aliwabwaga Nesserddine Nabi wa Yanga na George Lwandamina ya Azam.

Kwa ushindi huo John Bocco anakuwa mchezaji wa pili katika Ligi Kuu kutwaa tuzo hiyo ambapo awali ni Prince Dube pekee aliyekuwa anashikilia rekodi hiyo alipotwaa kwa mwezi Septemba mwaka jana na Mei mwaka huu wakati Adebayor alitwaa Mwezi Novemba Mwaka jana na Juni Mwaka huu.

Vilevile Didier Gomes wa Simba ambaye ametwaa tuzo hiyo kwa mara ya pili kwa mwezi April na Juni Mwaka huu na anaungana na aliyekuwa Kocha wa Yanga, Cedric Kaze ambaye alitwaa tuzo hiyo Mwezi Oktoba na Disemba mwaka jana na kuwa makocha pekee waliotwaa mara mbili tuzo hiyo.