Jumapili , 2nd Mei , 2021

Bondia bingwa wa zamani wa uzito wa juu Andy Ruiz Jr amenusurika kupoteza pambano kwa K.O ya mapema dhidi ya Chris Arreola, na baadae kufanikiwa kumshinda kwa kumzidi alama katika pambano liliofanyika katika jiji la California nchini Marekani.

Kibonge Andy Ruiz JR akimshushia kichapo Chriss Arreola

Ruiz Aliangushwa chini kwa konde zito la mkono wa kulia mapema tu katika raundi ya pili, lakini Raia huyo wa Mexico mwenye umri wa miaka 31 alirudi na kupambana vikali na kushinda kwa alama 117-110, 118-109 na 118-109 zilizotolewa kwenye kadi za alama za waamuzi wa pambano hilo.

Ikumbukwe Andy Ruiz Jr Alikuwa hajapigana tangu aliposhindwa kwenye pambano la marudiano dhidi ya Anthony Joshua mwezi Desemba 2019 baada ya hapo alipunguza uzito wa kilo 24.95 (55lb)

Ruiz sasa anashikilia rekodi ya kushinda mapambano 34 kati ya mapambano 36 aliyocheza, wakati Chris Arreola amepoteza mapambano yake 7 kati ya 48 aliyocheza akiwa na umri wa miaka 40 hivi sasa.