Jumanne , 11th Sep , 2018

Baada ya ripoti iliyochapishwa na jarida la Sunset la nchini Marekani, kueleza kuwa ni watu wachezaji sana katika nchi 100 zilizofanyiwa utafiti wana utaratibu wa kufanya mazoezi, mwalimu wa mazoezi Vanessa Alpha ameweka wazi sababu ya watu kutofanya mazoezi.

Waziri mkuu Kassim Majaliwa akifanya mazoezi

Akiongea kwenye MJADALA wa EATV Saa1 unaoruka kupitia East Africa Television, mwalimu huyo anayefundisha mazoezi kwenye 'gym' yake binafsi jijini Dar es salaam ametaja uvivu kama sababu kuu ya watu kutofanya mazoezi.

''Unajua watu hawafanyi mazoezi kwasababu ya uvivu japo wana visingizio vingi kama ratiba za kazi lakini ni uongo kwasababu zoezi linafanyika muda wowote na sehemu yoyote kinachotakiwa ni kujiwekea utaratibu tu'', amesema.

Vanessa amesisitiza kuwa kwenye mazoezi hakuna zoezi kubwa wala zoezi dogo bali kuna zoezi gumu na zoezi jepesi. Zoezi linakuwa gumu wakati wa kuanza na zoezi lolote linaweza kuwa jepesi pale tu mtu anapoliweza na kuwa kitu cha kawaida kwake.

Pia amewakumbusha watu kufanya mazoezi kwa matakwa yao binafsi kwani husaidia kuona zoezi ni jepesi tofauti na wale ambao hufanya kwa shinikizo pengine la mtu wake wa karibu au kushauriwa na daktari.