Jumamosi , 16th Jan , 2021

Mwimbaji wa muziki wa injili, Goodluck Gozbert, amesema kuwa yeye anaamini kwamba hadi pale atakapofikia wakati wa kuondoka duniani, atakuwa hajafanya kitu chochote ambacho kinatosheleza yale mema yote aliyofanyiwa na mama yake.

Mwimbaji wa muziki wa injili, Goodluck Gozbert

Kauli hiyo ameitoa wakati akizungumza kwenye kipindi cha DADAZ cha East Africa Television, na kuwasihi wale wote ambao mama zao wapo basi wahakikishe wanatenga muda kwa ajili ya mama zao, kama ambavyo MC Pilipili alivyokuwa akijitahidi kumpa muda mama yake.

"Mpaka siku naondoka Duniani nitakuwa sijaweza kumlipa kitu mama yangu, kuna wakati huwa namuomba Mungu angalau nipate muda wa kutoka na kutembea na mama, Mungu amlaze mahali pema Mama wa MC Pilipili, kwani alijitahidi kumpa muda, huwezi kumlipa mama eti kwa kusema umjengee nyumba eti ndiyo vitarudisha vitu ambavyo aliwahi kufanya", amesema Goodluck.

Aidha Goodluck ameongeza kuwa, "Kwa ambaye uko na mama na una muda unapata nafasi mtembelee sana mama, zungumza naye na cheka naye naamini ni vitu ambavyo huwezi kupata tena muda wa kuvifanya wakati ambapo siku zitakuwa zimesonga mbele".