Jumatatu , 7th Sep , 2015

Msanii wa muziki wa nchini Uganda, Rema Namakula ametolea ufafanuzi kurejea kwake nchini Uganda ghafla akivunja safari yake kuelekea Marekani, sababu pekee ikiwa ni kuzidiwa kuugua kwa mwanae mdogo Aamaal, na si uvunjaji wa taratibu za uhamiaji.

Msanii wa muziki wa nchini Uganda, Rema Namakula

Rema ambaye alikuwa akielekea katika onyesho New York Marekani ameeleza kuwa, amefikia uamuzi huo akiwa kama mzazi anayeamini hakuna kazi yoyote iliyo muhimu zaidi ya familia, na ujumbe uliomfikia katikati ya safari juu ya kuzidiwa kwa mwanae, ulimfanya kuacha mipango yote yake ya show.

Awali taarifa zimekuwa zikienezwa katika mitandao ya jamii kuwa msanii huyo alizuiwa katika uwanja wa ndege akijaribu kuingia Marekani kutokana hitilafu katika nyaraka zake za kusafiria, ikiwepo kutumia viza ya mualiko wa kutalii, wakati sababu hasa iliyompeleka ikiwa ni biashara ya show.

Hata hivyo, baadhi ya vyanzo bado vinashikilia msimamo kuwa Rema anajitetea tu na hakurudi nchini kwa kupenda hata kidogo.