Alhamisi , 8th Sep , 2016

Msanii Amini ambaye amewahi kufanya vizuri na ngoma kibao kali amefunguka na kusema kuwa kwa sasa yeye amekuwa akiishi kwa pesa ambazo anapata kwa kazi ya utunzi wa nyimbo mbalimbali za wasanii wa bongo fleva.

Amini

Amini alisema hayo kwenye kipindi cha 5Selekt kinachorushwa na ting'a namba moja kwa vijana EATV, ambapo amedai kuwa amekuwa akiwaandikia wasanii wengi nyimbo na yeye anafanya hivyo kwa kuwa anapenda lakini pia amekuwa akipata kipato ambacho kwa sasa ndiyo kinaendesha maisha yake.

"Unajua mimi suala la kuandika nyimbo ni kipaji changu, lakini pia kwa sasa naendesha maisha yangu kwa kazi ya kuandika nyimbo za wasanii mbalimbali. Muda mwingine naweza kutunga wimbo ambao nikifanya mimi unaweza usiwe 'hit' lakini nikimpa mtu mwingine ukafanya vizuri zaidi" alisema Amini

Kipindi cha nyuma Amini alikuwa anamuandikia sana nyimbo Linah Sanga ambaye alikuwa ni mpenzi wake lakini amedai kuwa kwa sasa hajaweza kuandika wimbo hata mmoja wa msanii huyo kutokana na ukweli kwamba Linah hajahitaji huduma hiyo kutoka kwake.