Jumatatu , 4th Dec , 2017

Msanii wa muziki wa kizazi kipya ambaye pia ni mkongwe, Godfrey Tumaini au Dudu Baya, ameshangazwa na kitendo cha msanii mwenzake Lucas Mkenda au Mr. Nice kusema anataka kumsaidia kimuziki, wakati mwenyewe yuko taaban hajiwezi.

Akifanya mahojiano na kipindi cha eNewz ya East Africa Television, Dudu Baya amesema hali ya Mr. Nice ni mbaya na yeye ndiye anayehitaji msaada, na sio kutangaza utajiri ambao anauota kama Dkt. Shika.

"Kauli zake za kuchekesha, mgonjwa mahututi bin taaban hawezi kumsaidia mtu mwenye afya njema, kwanza hata kauli zake mimi namjua vizuri, hali ya Mr. Nice ni mbaya sana kiafya mpaka kiuchumi, ameathirika kisaikolojia, ndio maana anaota maisha yake ya umaarufu ya kipindi kile, mpunga alioupiga kisha ukayeyuka, kuropoka kunisaidia mimi ni kama Dk Shika anayeota ana hela Urusi", amesema Dudu Baya.

Dudu Baya ameendelea kwa kusema kwamba msanii huyo sio msanii kwani hana uwezo wa kuandika nyimbo ambazo zinaweza kufanya vizuri sasa hivi, zaidi ya kuimba nyimbo ambazo zinaimbwa shuleni na watoto.