Alhamisi , 1st Jan , 2015

Mwenyekiti wa CUF Prof Ibrahim Lipumba pamoja na mbunge wa Kigoma kaskazini Mh Zitto Kabwe wamewataka wanachi wa mikoa ya kusini kutambua kuwa rushwa ndani ya serikali ya inayoongozwa na CCM haiwezi kuondoka.

Chama cha wananchi CUF kimewataka wanachi wa mikoa ya kusini kutambua kuwa suala la rushwa ndani ya serikali ni mfumo na katu hauwezi kuondoka iwapo viongozi wakuu serikalini wataendelea kufumbia macho ufisadi.

Mwenyekiti wa chama cha wananchi CUF taifa Ibrahimu Lipumba ametoa kauli hiyo katika mkutano mkubwa wa hadhara wa kuwashukuru wananchi wa mkoa wa Mtwara kwa kufanikisha ushindi katika chaguzi za serikali za mitaa vijiji na vitongoji kwa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi UKAWA katika baadhi ya maeneo ikiwemo manispaa ya Mtwara Mikindani.

Amesema viongozi wakuu serikalini wanafumbia macho rushwa na ufisadi unaofanyika serikalini hivyo kuendelea kuongozwa na serikali ya CCM ni sawa na kukumbatia maovu.

Naye mwenyekiti wa kamati ya kudumu ya bunge ya hesabu za mashirika ya umma Zitto Kabwe amesema wabunge wa vyama vya upinzani kwa umoja wao ndani ya bunge wataendelea kupambana na viongozi wabadhirifu.

Nao wabunge wa CUF wametaka wenyeviti wa serikali za mitaa vijiji na vitongoji watokanao na CUF kutobabaishwa na mamlaka nyingine.