Ijumaa , 23rd Aug , 2024

Serikali kupitia Wizara ya Afya imeendelea kujidhatiti katika kuchukua hatua za tahadhari dhidi ya ugonjwa wa Mpox kwa kutoa vielelezo vyenye jumbe zenye maudhui mbalimbali ya uelimishaji kuhusu ugonjwa huo katika mipaka mbalimbali ya nchi na viwanja vya ndege.

Hatua hiyo imeanza kuchukuliwa ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo aliyotoa Waziri wa Afya Mhe. Jenista Mhagama alipotembelea Kituo Jumuishi cha Forodha katika mpaka wa Namanga Mkoani Arusha wakati akikagua utayari na maandalizi ya kukabiliana na ugonjwa wa Mpox usiingie nchini.

Mkurugenzi wa Kinga Dkt. Ntuli Kapologwe pamoja na Mkurugenzi Msaidizi wa Sehemu ya Elimu ya Afya kwa Umma Dkt. Norman Jonas leo Agosti 23, 2024 wametoa vielelezo hivyo vyenye jumbe zenye maudhui mbalimbali ya uelimishaji kuhusu ugonjwa wa Mpox katika kiwanja cha ndege cha Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam ambapo baadhi ya vielelezo hivyo ni Video pamoja na vibango (Posters). 

Ikumbukwe kuwa licha ya ugonjwa wa Mpox kuripotiwa baadhi ya nchi jirani lakini Tanzania bado ni salama huku hatua mbalimbali za tahadhari zikichukuliwa.