Jumamosi , 17th Feb , 2018

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema serikali ya awamu ya tano itapambana na watu wanaotaka kuvuruga thamani ya zao la pamba, huku akiwataka wakulima wa zao hilo kuacha tabia ya kuchanganya mchanga au maji ndani ya pamba hizo kwani watakosa wanunuzi

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo wakati akizungumza kwa nyakati tofauti na wananchi wa wilaya ya Kwimba na kusema kumekuwa na tabia ya baadhi ya wakulima wasiokuwa waaminifu ambao kabla ya kuipeleka pamba sokoni wanachanganya na maji au mchanga.

"Wakulima msichezee pamba kwa kuichanganya na chochote ili kuiongezea uzito kwa sababu mtaharibu sifa nzuri ya pamba ya Tanzania ndani na nje ya nchi", amesema Waziri Majaliwa.

Aidha, Waziri Mkuu amesema serikali imeanza kuona tija tangu ilipoagiza maofisa kilimo katika mikoa inayolima pamba kusimamia kilimo hicho kuanzia ngazi za awali.

Akizungumzia kuhusu suala la wanunuzi wa pamba, Waziri Mkuu amesema tayari serikali imeweka mikakati ya kutosha itakayowezesha pamba yote kununuliwa na kuwaahidi wakulima hao kuwa ataangalia suala la bei katika soko la dunia na kisha kuwashawishi wanunuzi wanunue kwa bei nzuri itakayowanufaisha wakulima.