
Waziri wa Viwanda na Biashara Innocent Bashungwa
Waziri Bashungwa ameyabainisha hayo wakati wa ufunguzi wa wiki ya Viwanda na Biashara kwa nchi za SADC, uliohudhuriwa na viongozi kutoka nchi takribani 15, ukiongozwa na mwenyeji wao Rais Magufuli, na kusema kwamba Tanzania imekuwa ikifanya vizuri katika maonyesho hayo.
Bashungwa amebainisha kuwa, waonyeshaji wa bidhaa mbalimbali wako 1576 na kati ya hao watanzania wako 1404 na wanaotoka nje ya Tanzania wakiwa ni 172.
''Mh Rais Tanzania imekuwa ikifanya vizuri katika biashara ndani ya SADC, Takwimu zinaonyesha kuwa biashara ya mauzo ya Tanzania kwenda nchi za SADC kwa mwaka 2018 yalikuwa dola milioni 999.64, ikilinganishwa na dola milion 877.8 kwa mwaka 2017 hii ni sawa na ongezeko la asilimia 12.16''. Amesema Waziri Bashungwa.
Aidha Bashungwa amesema kuwa katika wiki hii ya viwanda Serikali ya Tanzania itakutana na viongozi ili kujadiliana changamoto zinazowakabili na kuzitafutia ufumbuzi ili kwa pamoja waweze kukuza maonyesho ya bidhaa.
''Uingizaji wa bidhaa kutoka SADC uliongezeka kutoka milion 600.64 kwa mwaka 2017 hadi kufikia milioni 604.32 kwa mwaka 2018, sawa na ongezeko la asilimia 0.61, bado kuna fursa kubwa ya kufanya biashara ndani ya nchi za Afrika na bado hatujazitumia na ninaamini kupitia wiki hii ya viwanda tutatumia muda mzuri mkutano huu, tutajadilia na kuweka mikakati na kujadiliana zile changamoto na kuzifungua'' amesema Waziri Bashungwa.
Maadhimisho ya kwanza ya maonyesho ya wiki ya Viwanda kwa nchi za SADC, yalifanyika nchini Eswatin kwa mwaka 2016, Afrika ya Kusini mwaka 2017, Namibia mwaka 2018 na Tanzania mwaka 2019.