Ijumaa , 9th Aug , 2024

Wafanyabaishara wa mazao ya chakula kwenye Soko la Ilala jijini Dar es Salaam, wameiomba Serikali kuadhimisha sikukuu ya wakulima kwa kuwawezesha kiuchumi ili wabadilishe maisha yao kupitia kilimo chao.

Glory Kalinga, mfanyabiashara wa mazao ya chakula, soko la Ilala jijini Dar es Salaam.

Wameyasema hayo jana kwenye kilele cha maadhimisho ya siku ya wakulina Agosti 8, 2024, wanasema madalali wamekuwa wakifata faida kubwa kuliko wakulima ambao wamekuwa wanawalangua kwa bei ndogo wakija huku mjini wanauza mazao kwa bei kubwa.
"Wakulima ndio wamekuwa wakivuja jasho na damu katika nyakati zote lakini kutokana na kutokuwa na itaji mikubwa wakija madalali wanawalangua kwa bei ya kudidimizwa mwisho wa siku wanakufa maskini",Glory Kalinga, Mfanyabiashara wa Mazao.

"Tunaomba tuboreshewe kwenye upatikanaji wa mbegu zilizo bora na zipatikane kwa wakati ili kuongeza tija kwenye uzalishaji wetu wa kila siku",Daudi Mkude, Mkulima na mfanyabiashara
"Tunaomba bei ya mazao iwe elekezi ili wazalishaji wakubwa waweze kunufaika kwa maana tunaona hawa watu wa kati ndio wanaofaidika lakini wakulima hawanufaiki kulingana na jitihada zao", Hamis Juma, Mfanyabiashara wa Mazao.

"Wakulima ndio ambao tungetamani kuwapazia sauti wao wakikosa mazao au mbegu bora ina maana hata sisi huku tutashindwa kupata bidhaa kwa wakati kwahiyo tungetamani wawezeshwe kwanza wao",alisema  Swaum Omary, Mfanyabiasha.

Sikukuu ya wakulima inayofahamika kuwa Nanenane ina sherekewa nchini kote tarehe 8 Agosti kila mwaka. Sherehe hiyo inatayarishwa na kuratibiwa na Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika kwa kushirikiana na Shirika la Chama cha Kilimo Tanzania (TASO) na kuhusisha Taasisi, Wizara na mtu mmoja mmoja wanaoshughulika na kilimo.
Mwanzo, sikukuu hii ya Nane Nane iliitwa ‘Saba Saba’ ambapo ilikuwa ikiadhimishwa kila tarehe 7 ya mwezi Julai. Baadaye ilihamishiwa Agosti, 8 ya kila mwaka baada ya Saba Saba kufahamika zaidi kwa maonyesho ya wafanyabiashara.

Sikukuu ya maonyesho ya wakulima iliadhimishwa kwa mara ya kwanza mwaka 1977 ili kuongezea nguvu sera ya Serikali ya wakati huo ya ‘ Siasa ni Kilimo ‘, ambapo wakulima katika wilaya, mkoa na kitaifa walionesha mazao yao halisi ya kilimo, wakaonyesha pembejeo za kisasa za killimo pamoja na kufundishwa namna ya kutumia pembejeo hizo kwa ustawi wa kilimo na taifa na kwa mwaka huu maadhimisho haya kitaifa yanafanyika katika mkoa wa Dodoma na mgeni Rasmi akiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dokta Samia Suluhu Hassan.