Jumatano , 14th Aug , 2024

Wananchi wa eneo la Bondeni lililoko Mbezi Beach A wilaya ya Kinondoni jijini Dar es salaam wameiomba serikali kupitia mkuu wa wilaya kuwahakikishia usalama wao dhidi ya vitendo vya uchimbaji mchanga pasipo kufuata utaratibu vinavyoendelea katika maeneo hayo yaliyopitiwa na mto 

Wakizungumza mbele ya mkuu wa wilaya ya Kinondoni Saad Mtambule wananchi hao wamesema hawapingi shughuli hizo za uchimbaji wa mchanga katika mto huo lakini wanapata hofu juu ya nini kitafuata baada ya mchanga huo kuchimbwa na mazingira yataachwa katika hali gani kwa sababu wapo ambao nyumba zao zipo karibu na mto huo na wanavyoendelea kuchimba mchanga wanawaweka hatarini zaidi

Akizungumza na wananchi hao Mkuu wa Wilaya Kinondoni Saad Mtambule amewataka wanaochimba mchanga kufuata taratibu katika zoezi hilo

"Tunatambua nchi yetu ina tatizo la ajira na vijana wengi wanahangaika kutafuta ajira lakini tunawakumbusha vijana kufanya shughuli ambazo hazivunji sheria na taratibu za nchi "

"Asilimia kubwa ya vijana wanaochimba mchanga hawafuati sheria wanachimba na kuondoka hawaachi mazingira vizuri kwa kupanda miti au kitu chochote ili kulinda eneo ambalo wamechimba mchanga Kwahiyo natoa wito kwa vijana kutafuta shughuli za halali na sio kuchimba mchanga kiholela" amesema Saad Mtambule ambaye ni Mkuu wa wilaya ya Kinondoni #EastAfricaRadio