Jumatano , 28th Aug , 2024

Jeshi la Polisi limesema wakati likiendelea na mahojiano na mgaga wa kienyeji Nkamba Kasubi kuhusu vifo vya watu watatu ambao miili yao imefukuliwa nyumbani kwake, jana Agosti 27, 2024 pia mganga huyo alikubali kuwaongoza polisi hadi kwenye mji wake mwingine uliopo Kijiji cha Porobanguma,

Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini DCP David Misime

wilayani Chemba mkoani Dodoma na kuonesha mashimo mengine sita.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Agosti 28 na Msemaji wa Jeshi la Polisi, David Misime imesema katika mashimo hayo mganga huyo na wenzake walifukia watu wengine wakiwemo watoto waliowaua na kuwazika na kufanya miili iliyofukuliwa kwa mganga kufikia tisa na mwili mwingine wa 10 ukiokotwa porini na kwamba tisa walizikwa kwa kukalishwa kwenye shimo kwa namna walivyosukumwa na imani zao za kishirikina isipokuwa mmoja aliyetupwa porini aliwe na wanyama.

"Baada ya taratibu za ufukuaji kufanyika ilipatikana miili ya Seni Jishabi (28), mkazi wa Kijiji cha Porobanguma ambaye alipotea toka Machi 3, 2024 na walidai kumuua na kumzika Aprili 2024, Mohamed Juma (27), Mkazi wa Nyamikumbi A mkoa wa Singida ambaye alipotea Mei 15, 2024 na wao wameeleza walimuua kwa kumnyonga kisha kumzika, Daudi Msanku (27), Mkazi wa Gawidu Mkoani Manyara ambaye alipotea Mei 27, 2024 na baada ya kumuua walichoma mwili wake moto kisha majivu yake kuyahifadhi kwenye ndoo, huyu ndiye ambaye pikipiki yake alikamatwa nayo Miraji Shabani Nyalandu akijaribu kutoroka baada ya kuona watuhumiwa wenzake wanakamatwa mfululizo na Askari Polisi," imeeleza taarifa ya polisi

Aidha taarifa hiyo imeongeza kuwa, "Mwingine ni Ramadhan Yusuph (26), mkazi wa Kidika Manyara, ambaye walimuua April 2024, Mwekwa Kasubi (umri miezi 4), mtoto huyu ni wa huyo Mganga wa kienyeji ambapo aliuawa Machi 2023, Maka Selemani Shabani Nyalandu (umri miezi miwili), aliuawa Juni 2023 na ni mtoto wa mtuhumiwa Selemani Shabani Nyalandu maarufu Hango, watoto hawa walizikwa wakiwa hai kwenye zizi la mifugo, pia watuhumiwa walikiri kumuua Ramadhani Bakari Kilesa (80), Mkazi wa Porobanguma na kutupa mwili wake katika Pori la Akiba Swangaswanga, maiti yake ilipatikana Julai 25, 2024 lakini ilikuwa haijabainika kuwa aliuawa na watuhumiwa hawa hadi jana walipokiri kumuua na kueleza sehemu walipomtupa ili mwili wake uliwe na wanyamapori,"

DCP Misime ameongeza kuwa miili ya watu hao wote 10 iliyopatikana mkoani Singida ni mitatu (3) na Dodoma ni saba (7).