Jumatano , 27th Jul , 2016

Jeshi la Polisi Mkoani Kilimanjaro linawashikilia watuhumiwa 15 wakiwemo askariwa zamani wa jeshi hilo kwa tuhuma mbalimbali za unyang'anyi wa kutumia silaha na kutumia nguvu pamoja na matumizi ya dawa za kulevya.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro Wilbroad Mutafungwa

Akizungumza na waandishi wa Habari ofisini kwake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro Wilbroad Mutafungwa amesema askari hao walifukuzwa na jeshi la Polisi kati ya mwaka 2013 na 2015 baada ya kubainika kujihusisha na ujambazi pamoja na mauaji.

Kamanda mtafungwa amewataja watuhumiwa hao waliowahi kuwa askari polisi wa jeshi hilo ni Jackos Zenzule Mkazi wa Mabogini pamoja na Elihuruma Mringi Mkazi wa Bomang,ombe ambao wanathumiwa na matukio ya ujambazi pamoja na mauaji ya raia.

Jeshi la Polisi pia linamshirikia Mwanamke mmoja anaejulikana kwa jina la Lightness Wilfred Mkazi wa Kiboriloni Mjini Moshi, ambae amekiri kupanga tukio la ujambazi lililotokea mwishoni mwa wiki katika duka la mfanyabiashara wa mitumba Clement Mbowe, na kufanikiwa kupora milioni 10 ambazo ni mauzo ya mitumba.

Katika tukio jingine jeshi la Polisi limewakamata raia wawili wa Kenya Edward Kimata, na Crispin Kanywela, kwa kujihusisha na matukio ya wizi ndani ya benki kwa kuwabadilishia wateja bahasha zenye fedha na zenye karatasi.