
Watu sita wanashikiliwa na Jeshi la polisi Mkoani Shinyanga kwa tuhuma za kutorosha madini ya dhahabu yenye uzito wa gramu 930. 88 ambayo thamani yake ni Sh Milioni 93
Kamanda wa Jeshi la polisi Mkoani Shinyanga Janeth Magomi amesema watuhumiwa hao ambao majina yao yamehifadhiwa kwa uchunguzi zaidi,wamekamatwa na askari katika barabara ya Ilogi Kata ya Bugarama wilayani Kahama inayoelekea mkoa jirani wa Geita baada ya askari kulitilia mashaka gari lenye namba za usajili T 913 DRX Toyota Land Cruiser na kulifuatilia.
Baada ya gari hilo kukamatwa na askari waliokuwa doria walikuta watu sita ndani ya gari na walipofanya upekuzi walikuta madini ya dhahabu, pesa taslimu Sh Milioni 97,025,000, mzani wa kielekitroniki wa kupimia dhahabu pamoja na mashine moja ya kupima ubora wa dhahabu.