Ijumaa , 22nd Mei , 2015

Mwili wa marehemu Basili Mwalongo (24) umesusiwa kuzikwa na wananchi wa kijiji cha Lugenge Mkoani Njombe kutokana na mwili huo kukosa kibali na muhuri wowote kutoka serikalini na kuonesha sababu ya kifo chake.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Njombe Franco Kibona.

Inasadikiwa mtu huyo amekufa kwa kupigwa na risasi akiwa na wenzake katika kilabu cha pombe maeneo ya Nzengelentete mtaa wa kambarage Njombe mjini na kusababisha majeruhi kwa mwenzake Fred Sanga ambaye mpaka sasa anaendelea kupatiwa matibabu katika hospitali ya Kibena.

Marehemu Mwalongo ambaye ilitakiwa azikwe jana nyumbani kwao katika kijiji na kata ya Lugenge, hivyo mazishi hayo kushindwa kufanyika na kuahirishwa kutokana na kugundua kibali hicho kutokuwa na muhuri na kuonesha sababu ya kifo cha marehemu huyo.

Chombo hiki kimefanikiwa kukiona kibali hicho kilicho tolewa na hospitali ya Kibena ambacho ni kibali cha mazishi huku mahali pa kuandika sababu ya kifo cha marehemu pakiwa hapajaandikwa kitu.

Akizungumza na Chombo hiki msemaji wa familia ya marehemu Mwalongo, Joseph Mwalongo, amesema wamegoma kuuzika mwili huo kufuatia dosari zilizojitokeza katika kibali hicho, na kwamba kama serikali kupitia ofisi ya mkuu wa mkoa haitarekebisha kibali hicho watairudisha maiti kituo cha polisi ili wazike wenyewe wanavyojua.

Naye mmoja wa shuhuda wa tukio hilo la kususiwa mwili wa marehemu kuzikwa Rose Mayemba, amesema wananchi walifikia maamuzi ya kususia mazishi hayo kutokana na polisi kushindwa kutuma uwakilishi kama walivyoafikiana jana katika kikao cha ulinzi na usalama juzi.

Amesema kuwa wanakijiji hawakujua baada ya mazishi nini kutatokea kutona na kibali kilichotolewa kutokuwa na mhuri na sahihi za viongozi hali iliyozua sintofahamu hadi kupelekea kuundwa tume ya watu nane kwenda Mkuu wa Wilya ya Njombe Sarah Dumba ili kujua hatua ya jambo hilo.

Wananchi hao baada ya kushindwa kuzika maiti hiyo waliunda kamati ya watu kwaajili ya kwenda kufuatilia kibali kilicho kamilika kwa mkuu wa wilaya ya Njombe Sarah Dumba, na kuwa kibali halali kisipo patikana wananchi watabeba maiti hiyo na kuipeleka katika jeshi la Polisi.

Kwa upande wake kamanda wa polisi mkoa wa Njombe Franco Kibona alipofuatwa kutolea ufafanuzi wa tukio hilo alionesha ukali kwa waandishi wa habari na kuwataka kuwa atatoa ufafanuzi siku ya leo huku akisema kuwa ana kikao na na kuna mambo bado hayajakamilika.