Ijumaa , 30th Sep , 2022

Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amesema matatizo mengi yanayiowakumba vijana nchini kwa sasa kiafya yanatokana na lishe duni huku matatizo hayo yakiendelea kuwa siri

Rais Samia amewataka watafiti mbalimbali kujikita kufanya utafiti na kuja na majibu sahihi kuhusu changamoto ya afya hususani kwa vijana nchini ambao amesema wanahangaika sana unapofika muda wa kuzalisha 

"Kwanini watoto wetu wakifika wakati wa kuongeza jamii wanahangaika, mara supu ya pweza, tuna tatizo na mnalijua mnalificha watafiti fanyeni utafiti, na kwasababu halisemwi ni siri linaumiza zaidi vijana wetu, tatizo kubwa lipo kwenye lishe"

Aidha amesema kama hali hiyo haitatafutiwa suluhu basi hali itaendelea kuwa mbaya zaidi 

"Tukiacha hali ikienda hivo tunaenda kuwa na taifa goigoi, tunaenda kuwa na taifa lenye watu lakini sio rasilimali watu, ni watu ambao ni mzigo kwa taifa, na sio watu ambao watazalisha kwa ajili ya taifa" 

Hata hivyo Rais samia amesema pamoja na changamoto ya lishe duni nchini lakini bado kuna changamoto kubwa ya lishe iliyopitiliza ambayo pia inawasumbua watu wengi

Utafiti wa lishe uliofanyika mwaka 2018 unaonesha kuwa wakati Tanzania inapambana na matatizo yanayotokana na lishe pungufu, kwa upande mwingine kuna matatizo yanayotokana na lishe inayopitiliza, tuna vitambi, wataalamu mnapaswa kulitekeleza

Rais Samia amesema hayo leo Ijumaa Septemba 30 wakati akishughudia utiaji saini mkataba wa usimamiaji wa shughuli za lishe  Jijini dodoma