Jumanne , 30th Jul , 2024

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega amesema mpaka sasa mradi wa ujenzi wa bandari ya uvuvi ya Kilwa Masoko umeshatoa ajira kwa vijana wapatao 570 ambao wanafanyakazi hapo huku akiongeza kuwa utakapokamilika utatoa ajira elfu 30 katika nyanja mbalimbali.

Waziri Ulega amesema hayo leo alipotembelea kukagua maendelea ya ujenzi wa mradi huo unaofanyika wilayani Kilwa, mkoani Lindi leo Julai 30, 2024.

"Leo nimekuja kutembelea huu mradi nimewakuta vijana wanafurahia kazi wanayoifanya, vijana wa Taifa zima watapata fursa ya kufanya, tunataraji vijana wasiopungua elfu 30  kutoka maeneo mbalimbali watapata ajira hapa, tunamshukuru Mhe. Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mradi huu ambao ni wa kilelezo kwa Taifa letu," amesema Waziri Ulega.

Aidha Waziri huyo ameridhishwa na maendeleo ya ujenzi wa Bandari ya Uvuvi ya Kilwa Masoko ambao mpaka sasa umefikia asilimia 63 na unatarajiwa kukamilika mwezi Februari, 2025.

Amesema bandari hiyo ya uvuvi inayojengwa kwa fedha za ndani ni mradi wa kielelezo unaotekelezwa chini ya serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan.